Add parallel Print Page Options

Paulo Aitetea Huduma yake

10 Mimi, Paulo, ninawasihi kwa unyenyekevu na upole wa Kristo. Wengine wanasema kuwa nina ujasiri ninapowaandikia nikiwa mbali, lakini ni mwoga kusema jambo lo lote ninapokuwa pamoja nanyi. Wanadhani sababu ya kutenda yale tunayoyafanya ni kama zile za kidunia. Ninapanga kuwa jasiri sana kinyume chao watu hao hapo ninapokuja kwenu. Tafadhali ninawaomba, sitahitaji kutumia ujasiri huo kwenu. Tunaishi katika ulimwengu huu, lakini hatupigani vita yetu kama ulimwengu unavyopigana. Silaha tunazozitumia si za kibinadamu. Silaha zetu zina nguvu kutoka kwa Mungu na zinaweza kuharibu ngome za adui. Tunaharibu mabishano ya watu, na tunasambaratisha kila wazo la kiburi linalojiinua kinyume cha elimu ya Mungu. Pia tunateka kila wazo na kulitiisha ili limtii Kristo. Tuko tayari kumwadhibu kila mtu asiyetii, lakini tunataka ninyi muwe watiifu ipasavyo kwanza.

Mnatakiwa kuchunguza ukweli halisi wa mambo ulio mbele ya macho yenu. Ikiwa mna uhakika kuwa ninyi ni wa Kristo, mnapaswa kukumbuka kuwa na sisi ni wa Kristo kama ninyi mlivyo wa Kristo. Inaweza kuonekana kana kwamba tunajivuna sana kupita kiasi kidogo kuhusu mamlaka ambayo Bwana ametupa sisi. Lakini alitupa mamlaka hii ili kuwatia nguvu ninyi, na sio kuwaumiza. Hivyo sitaona haya kwa lolote ambalo tumejisifu kwalo. Sitaki mfikiri kuwa najaribu kuwatisha kwa barua zangu. 10 Wengine wanasema, “Barua za Paulo zina shuruti na matakwa mengi, Lakini anapokuwa pamoja nasi, ni mdhaifu na msemaji asiyefaa.” 11 Watu hao wanapaswa kulielewa jambo hili: tutakapokuwa pamoja nanyi, tutatenda mambo kwa ujasiri ule ule tunaouonyesha sasa katika barua zetu.

12 Hatujaribu kujiweka katika daraja moja na wale wanaojisifu wenyewe. Hatujilinganishi na watu hao. Wao wanatumika wenyewe kwa kujipima wenyewe, na wanajilinganisha miongoni mwao wenyewe. Hili linadhihirisha kuwa hawajui lolote.

13 Lakini hatutajisifia lolote nje ya kazi tuliyopewa kuifanya. Tutaweka ukomo wa kujisifia kwetu katika kazi aliyotupa Mungu kuifanya, lakini kazi hii inajumuisha kazi yetu kwenu. 14 Tungekuwa tunajivuna zaidi na zaidi ikiwa tungekuwa hatujafika kabisa kwenu. Lakini tulikuwa wa kwanza kufika kwenu na Habari Njema ya Kristo. 15 Tumeweka ukomo wa kujivuna kwetu katika kazi ambayo ni yetu. Hatujivunii kazi ambayo wameifanya watu wengine. Tunatumaini kuwa imani yenu itaendelea kukua. Tunatumaini kuwa mtaisadia kazi yetu kukua zaidi na zaidi. 16 Tunataka kuieneza habari njema katika maeneo ya mbali zaidi kupita mji wenu. Hatutaki kujisifia juu ya kazi ambayo imefanywa na mtu mwingine katika eneo lake. 17 “Yeyote anayejisifu na ajisifu juu ya Bwana tu.”(A) 18 Kile watu wanachosema kuhusu wao wenyewe hakina maana yeyote. Cha muhimu ni ikiwa Bwana anasema kuwa wamefanya vizuri.