Add parallel Print Page Options

Yesu ni Bwana Juu ya Siku ya Sabato

(Mt 12:1-8; Mk 2:23-28)

Wakati fulani siku ya Sabato, Yesu alikuwa akitembea kupitia katika baadhi ya mashamba ya nafaka. Wafuasi wake wakachukua masuke, wakayapukusa mikononi mwao na kula nafaka. Baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, “Kwa nini mnafanya hivyo? Ni kinyume na Sheria ya Musa kufanya hivyo siku ya Sabato.”

Yesu akawajibu, “Je, mmesoma kuhusu jambo alilofanya Daudi, wakati yeye na watu wake walipohisi njaa? Daudi alikwenda katika nyumba ya Mungu, akachukua mikate iliyotolewa kwa Mungu na kuila. Na kuwapa wenzake baadhi ya mikate hiyo. Hii ilikuwa kinyume na Sheria ya Musa, inayosema kuwa makuhani pekee ndiyo wanaoruhusiwa kula mikate hiyo.” Kisha Yesu akawaambia Mafarisayo, “Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa Sabato.”

Yesu Amponya Mtu Siku ya Sabato

(Mt 12:9-14; Mk 3:1-6)

Siku nyingine ya Sabato Yesu aliingia katika sinagogi na kuwafundisha watu. Katika sinagogi hili alikuwemo mtu aliyepooza mkono wake wa kulia. Walimu wa sheria na Mafarisayo walikuwa wakimvizia Yesu. Walikuwa wanasubiri waone ikiwa ataponya siku hiyo ya Sabato. Walitaka kumwona akifanya jambo lolote lililo kinyume ili wamshitaki. Lakini Yesu alijua walilokuwa wanawaza. Akamwambia mtu mwenye mkono uliopooza, “Nyenyuka na simama hapa ambapo kila mtu anaweza kukuona!” Yule mtu akanyenyuka na kusimama pale. Ndipo Yesu akawaambia, “Ninawauliza ninyi, Sheria inaturuhusu tufanye nini siku ya Sabato: kutenda mema au kutenda mabaya? Je, ni halali kuokoa uhai au kuuangamiza?”

10 Yesu akawatazama watu wote kila upande, kisha akamwambia yule mtu, “Nyoosha mkono wako.” Akaunyosha mkono wake, na akaponywa. 11 Mafarisayo na walimu wa sheria wakakasirika sana kiasi cha kutofikiri sawasawa, wakashauriana wao kwa wao wamfanye nini Yesu.

Yesu Achagua Wanafunzi Wake Kumi na Wawili

(Mt 10:1-4; Mk 3:13-19)

12 Siku chache baadaye, Yesu alikwenda mlimani kuomba. Alikaa huko usiku kucha akimwomba Mungu. 13 Asubuhi iliyofuata aliwaita wafuasi wake, akachagua kumi na wawili miongoni mwao na kuwaita Mitume. Nao ni:

14 Simoni (ambaye Yesu alimwita Petro),

Andrea aliyekuwa kaka yake Petro,

Yakobo,

Yohana,

Filipo,

Bartholomayo,

15 Mathayo na

Tomaso,

Yakobo mwana wa Alfayo,

Simoni aliyeitwa Mzelote,

16 Yuda mwana wa Yakobo,

na Yuda Iskariote (yule ambaye baadaye alimsaliti Yesu).

Yesu Afundisha na Kuponya Watu

(Mt 4:23-25; 5:1-12)

17 Yesu na mitume wakatelemka kutoka mlimani. Yesu akasimama mahali tambarare. Kundi kubwa la wafuasi wake lilikuwa pale. Walikuwepo pia watu wengi waliotoka sehemu zote za Uyahudi, Yerusalemu, na maeneo ya pwani karibu na Tiro na Sidoni. 18 Wote walikuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao. Aliwaponya watu waliokuwa wanasumbuliwa na mapepo. 19 Kila mtu alijaribu kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa unamtoka. Yesu aliwaponya wote.

20 Yesu akawatazama wafuasi wake na kusema,

“Heri ninyi mlio maskini.
    Maana Ufalme wa Mungu ni wenu.
21 Heri ninyi mlio na njaa sasa.
    Maana mtashibishwa.
Heri ninyi mnaolia sasa.
    Maana mtafurahi na kucheka.

22 Watu watawachukia kwa sababu ninyi ni wa milki ya Mwana wa Adamu. Watawabagua na watawatukana. Watajisikia vibaya hata kutamka majina yenu. Mambo haya yatakapotukia, mjue kuwa baraka kuu ni zenu. 23 Ndipo mfurahi na kurukaruka kwa furaha, kwa sababu mna thawabu kuu mbinguni. Baba zao waliwafanyia manabii vivyo hivyo.

24 Lakini ole wenu ninyi matajiri,
    kwa kuwa mmekwishapata maisha yenye raha.
25 Ole wenu ninyi mlioshiba sasa,
    kwa kuwa mtasikia njaa.
Ole wenu ninyi mnaocheka sasa,
    kwa kuwa mtalia na kuhuzunika.

26 Ole wenu watu wote wanapowasifu ninyi. Maana mababu zao waliwasifu manabii wa uongo vivyo hivyo daima.

Wapende Adui Zako

(Mt 5:38-48; 7:12a)

27 Lakini ninawaambia ninyi mnaonisikiliza, wapendeni adui zenu. Watendeeni mema wale wanaowachukia. 28 Mwombeni Mungu awabariki wale wanaowalaani ninyi, waombeeni wale wanaowaonea. 29 Mtu akikupiga shavu moja, mwache akupige na la pili pia. Mtu akichukua koti lako, usimkataze kuchukua shati pia. 30 Mpe kila akuombaye kitu. Mtu yeyote akichukua kitu chako, usitake akurudishie. 31 Watendeeni wengine kama mnavyotaka wao wawatendee ninyi.

32 Je, msifiwe kwa sababu ya kuwapenda wale wanaowapenda ninyi tu? Hapana, hata wenye dhambi, wanawapenda wale wanaowapenda. 33 Je, msifiwe kwa kuwa mnawatendea mema wale wanaowatendea mema ninyi? Hapana, hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo! 34 Je, msifiwe kwa kuwa mnawakopesha watu kwa kutarajia kupata vitu kutoka kwao? Hapana, hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi wengine, ili warudishiwe kiasi kile kile!

35 Ninawaambia kuwa wapendeni adui zenu na kuwatendea mema. Wakopesheni watu bila kutarajia kitu kutoka kwao. Mkifanya hivyo, mtapata thawabu kuu. Mtakuwa wana wa Mungu Mkuu Aliye Juu. Ndiyo kwa sababu Mungu ni mwema hata kwa wenye dhambi na wasiomshukuru. 36 Iweni na upendo na huruma, kama Baba yenu alivyo.

Iweni Waangalifu Mnapokosoa Wengine

(Mt 7:1-5)

37 Msiwahukumu wengine, nanyi hamtahukumiwa na Mungu. Msiwalaani wengine nanyi hamtalaaniwa. Wasameheni wengine nanyi mtasamehewa. 38 Wapeni wengine vitu, nanyi mtapokea. Mtapewa vingi; kipimo chenye ujazo wa kusukwasukwa na kumwagika. Mungu atawapa ninyi kwa kadri mnavyotoa.”

39 Yesu akawaambia mfano huu, “Je, asiyeona anaweza kumwongoza asiyeona mwenzake? Hapana. Wote wawili watatumbukia shimoni. 40 Wanafunzi si bora kuliko mwalimu wao. Lakini wakiisha kufundishwa na kuhitimu, wanakuwa kama mwalimu wao.

41 Kwa nini unaona kipande kidogo cha vumbi kilicho katika jicho la rafiki yako, lakini hujali kipande cha ubao kilicho ndani ya jicho lako mwenyewe? 42 Unawezaje kumwambia rafiki yako, ‘Hebu nikitoe kipande cha vumbi kilicho katika jicho lako’? Je, huwezi kukiona kipande cha ubao kilicho katika jicho lako mwenyewe? Wewe ni mnafiki. Kwanza kitoe kipande cha ubao katika jicho lako, ndipo utaona vyema na utaweza kukitoa kipande cha vumbi kilicho katika jicho la rafiki yako.

Yale Unayofanya Yanaonesha Jinsi Ulivyo

(Mt 7:17-20; 12:34b-35)

43 Mti mzuri hauzai matunda mabaya. Na mti mbaya hauzai matunda mazuri. 44 Kila mti unatambuliwa kutokana na aina ya matunda unayozaa. Huwezi kupata tini kwenye vichaka vya miiba. Na huwezi kuchuma zabibu kwenye michongoma! 45 Watu wema wana mambo mazuri katika mioyo yao. Ndiyo sababu hutamka mambo mema. Lakini waovu wana mioyo iliyojaa uovu, na ndiyo sababu hutamka mambo maovu. Mambo wanayotamka watu katika midomo yao, ndiyo yaliyojaa katika mioyo yao.

Aina Mbili za Watu

(Mt 7:24-27)

46 Kwa nini mnaniita, ‘Bwana, Bwana’ lakini hamtendi kama ninavyosema? 47 Nitawaonesha namna walivyo watu wanaokuja kwangu, wale wanaoyasikia na kuyatii mafundisho yangu. 48 Ni kama mtu anayejenga nyumba, huchimba chini sana, na kujenga nyumba yake kwenye mwamba. Mafuriko yanapokuja, huigonga nyumba kwa nguvu, nyumba hiyo haiwezi kuanguka kwa kuwa imejengwa vizuri.

49 Lakini watu wanaoyasikia maneno yangu na hawayatii ni kama mtu anayejenga nyumba bila kutayarisha msingi. Mafuriko yanapokuja, nyumba huanguka chini kwa urahisi na kubomoka kabisa.”