Add parallel Print Page Options

Jitoe Mwenyewe kwa Mungu

Mapigano na magombano yanatokea wapi miongoni mwenu? Je, hayatoki kutoka ndani yenu wenyewe, kutoka katika tamaa zenu za starehe ambazo zinafanya vita siku zote ndani ya miili yenu? Mnataka mambo lakini hamyapati, hivyo mnaua na mnakuwa na wivu juu ya watu wengine. Lakini bado hamwezi kuyafikia mnayoyataka, hivyo mnagombana na kupigana. Nanyi ndugu zangu hampokei mambo mnayoyataka kwa sababu hamumwombi Mungu. Na mnapoomba, lakini hampokei cho chote kwa sababu mnaomba kwa dhamiri mbaya, ili muweze kuvitumia mlivyopatiwa kwa anasa zenu.

Watu msio waaminifu, hamjui kwamba kuupenda ulimwengu ni sawa na kumchukia Mungu? Yeyote anayetaka kuwa rafiki wa dunia hujifanya mwenyewe kuwa adui wa Mungu. Je, kile Maandiko yanachokisema hakina maana yoyote kwenu? Ile roho ambayo Mungu aliifanya ikae ndani yetu wanadamu imejaa tamaa yenye wivu? Lakini Mungu ametuonesha sisi, rehema kuu zaidi. Ndiyo maana Maandiko yanasema:

Mungu huwapinga wenye kiburi,
    lakini huwapa neema wale walio wanyenyekevu.(A)

Kwa hiyo jiwekeni chini ya Mungu. Mpingeni Shetani naye atawakimbia ninyi. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Iosheni mikono yenu ninyi wenye dhambi na kuitakasa mioyo yenu enyi wanafiki! Ombolezeni na kulia! Kicheko chenu na kigeuzwe kuwa maombolezo, na furaha yenu igeuzwe kuwa huzuni kubwa. 10 Jinyenyekezeni chini ya Bwana, naye atawainua juu.

Wewe Siyo Hakimu

11 Ndugu, msiendelee kukosoana ninyi kwa ninyi. Yeye anayemnenea mabaya ndugu yake au anayemhukumu ndugu yake atakuwa anailaumu Sheria na atakuwa anaihukumu Sheria. Na kama utaihukumu Sheria, hautakuwa unafanya yale yanayosemwa na Sheria, bali utakuwa ni hakimu. 12 Kuna Mtoa Sheria mmoja tu na hakimu, ndiye Mungu aliye na uwezo wa kuokoa na kuangamiza. Hivyo wewe unafikiri ni nani, wewe unayemhukumu jirani yako?

Mwache Mungu Apange Maisha Yako

13 Sikilizeni mnaosema, “Leo au kesho tutasafiri kwenda kwenye mji huu au ule, na tutakaa mwaka mzima pale, tutafanya biashara hapo na kujipatia fedha nyingi.” 14 Hamjui hata yatakayotokea katika maisha yenu kesho yake tu. Kwani ninyi ni mvuke tu ambao huonekana kwa kipindi kifupi tu kisha hutoweka. 15 Badala yake, nyakati zote mngesema, “Kama Bwana anapenda, tutaishi na tutafanya hivi au vile.” 16 Kama ilivyo, ninyi mna kiburi na kujivuna. Majivuno yote ya jinsi hiyo ni uovu! 17 Hivyo sasa, mnaposhindwa kufanya mliyoyajua ni haki, mtakuwa na hatia ya dhambi.