Add parallel Print Page Options

Mwanamke Ampa Yesu Heshima

(Mt 26:6-13; Mk 14:3-9)

12 Siku sita kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu alienda Bethania. Huko ndiko alikoishi Lazaro, yule mtu aliyefufuliwa na Yesu kutoka wafu. Hapo walimwandalia Yesu karamu ya chakula. Naye Martha alihudumu na Lazaro alikuwa mmoja wa watu waliokuwa wakila chakula pamoja na Yesu. Mariamu akaleta manukato ya thamani sana yaliyotengenezwa kwa nardo asilia kwenye chombo chenye ujazo wa nusu lita[a] hivi. Akayamwaga manukato hayo miguuni mwa Yesu. Kisha akaanza kuifuta miguu ya Yesu kwa nywele zake. Harufu nzuri ya manukato hayo ikajaa nyumba nzima.

Yuda Iskariote, mmoja wa wafuasi wa Yesu, naye alikuwepo hapo. Yuda ambaye baadaye angemkabidhi Yesu kwa maadui zake akasema, “Manukato hayo yana thamani ya mshahara wa mwaka[b] wa mtu. Bora yangeuzwa, na fedha hizo wangepewa maskini.” Lakini Yuda hakusema hivyo kwa vile alikuwa anawajali sana maskini. Alisema hivyo kwa sababu alikuwa mwizi. Naye ndiye aliyetunza mfuko wa fedha za wafuasi wa Yesu. Naye mara kadhaa aliiba fedha kutoka katika mfuko huo.

Yesu akajibu, “Msimzuie. Ilikuwa sahihi kwake kutunza manukato haya kwa ajili ya siku ya leo; siku ambayo maziko yangu yanaandaliwa. Nyakati zote mtaendelea kuwa pamoja na hao maskini.[c] Lakini si kila siku mtakuwa pamoja nami.”

Mpango Dhidi ya Lazaro

Wayahudi wengi wakasikia kwamba Yesu alikuwa Bethania, Kwa hiyo walienda huko ili wakamwone. Walienda pia ili kumwona Lazaro, yule ambaye Yesu alimfufua kutoka wafu. 10 Viongozi wa makuhani nao wakafanya mpango wa kumuua Lazaro. 11 Walitaka kumwua kwa sababu, Wayahudi wengi waliwaacha makuhani hao na kumwamini Yesu.

Yesu Anaingia Yerusalemu Kama Mfalme

(Mt 21:1-11; Mk 11:1-11; Lk 19:28-40)

12 Siku iliyofuata watu waliokuwamo Yerusalemu walisikia kwamba Yesu alikuwa anakuja huko. Hili ni kundi la watu waliokuja kusherehekea sikukuu ya Pasaka. 13 Hawa walibeba matawi ya miti ya mitende na kwenda kumlaki Yesu. Pia walipiga kelele wakisema,

“‘Msifuni[d] Yeye!’
‘Karibu! Mungu ambariki yeye
    ajaye kwa jina la Bwana!’(A)
Mungu ambariki Mfalme wa Israeli!”

14 Yesu akamkuta punda njiani naye akampanda, kama vile Maandiko yanavyosema,

15 “Msiogope, enyi watu wa Sayuni![e]
Tazameni! Mfalme wenu anakuja.
    Naye amepanda mwana punda.”(B)

16 Wafuasi wa Yesu hawakuyaelewa yale yaliyokuwa yanatokea wakati huo. Lakini Yesu alipoinuliwa juu kwenye utukufu, ndipo walipoelewa kuwa haya yalitokea kama ilivyoandikwa juu yake. Kisha wakakumbuka kwamba walifanya mambo haya kwa ajili ya Yesu.

17 Siku Yesu alipomfufua Lazaro kutoka wafu na kumwambia atoke kaburini walikuwepo watu wengi pamoja naye. Hawa walikuwa wakiwaeleza wengine yale aliyoyafanya Yesu. 18 Ndiyo sababu watu wengi walienda ili kumlaki Yesu; kwa kuwa walikuwa wamesikia habari za ishara hii aliyoifanya. 19 Mafarisayo nao wakasemezana wao kwa wao, “Tazameni! Mpango wetu haufanyi kazi. Watu wote wanamfuata Yesu!”

Yesu Azungumza Juu Uzima na Kifo

20 Hapo Yerusalemu walikuwepo pia Wayunani. Hawa walikuwa ni miongoni mwa watu walioenda mjini humo kuabudu wakati wa sikukuu ya Pasaka. 21 Hao walimwendea Filipo, aliyetoka Bethsaida kule Galilaya. Wakasema, “Bwana, tunahitaji kumwona Yesu.” 22 Filipo alienda na kumwambia Andrea hitaji lao. Kisha Andrea na Filipo walienda na kumwambia Yesu.

23 Yesu akawaambia Filipo na Andrea, “Wakati umefika kwa Mwana wa Adamu kuupokea utukufu wake. 24 Ni ukweli kwamba mbegu ya ngano inapaswa kuanguka katika ardhi na kuoza kabla ya kukua na kuzaa nafaka nyingi ya ngano. Kama haitakufa, haitaongezeka zaidi ya hiyo mbegu moja. 25 Yeyote anayeyapenda maisha yake aliyonayo atayapoteza. Yeyote atakayetoa maisha yake kwa Yesu katika ulimwengu huu atayatunza. Nao wataupata uzima wa milele. 26 Kama mtu atanitumikia inampasa anifuate. Watumishi wangu watakuwa pamoja nami popote nitakapokuwa. Mtu atakayenitumikia Baba yangu atamheshimu.

Yesu Azungumza Kuhusu Kifo Chake

27 Sasa ninapata taabu sana rohoni mwangu. Nisemeje? Je, niseme, ‘Baba niokoe katika wakati huu wa mateso’? Hapana, nimeufikia wakati huu ili nipate mateso. 28 Baba yangu, ufanye yale yatakayokuletea wewe utukufu!”

Kisha sauti kutoka mbinguni ikasikika ikisema, “Tayari nimekwisha upata utukufu wangu. Nitaupata tena.”

29 Watu waliokuwa wamesimama hapo wakaisikia sauti hiyo. Wakasema ilikuwa ni ngurumo. Lakini wengine wakasema, “Malaika amesema naye!”

30 Yesu akasema, “Sauti hiyo ilikuwa ni kwa ajili yenu si kwa ajili yangu. 31 Sasa ni wakati wa ulimwengu kuhukumiwa. Sasa mtawala wa ulimwengu[f] huu atatupwa nje. 32 Nami nitainuliwa juu[g] kutoka katika nchi. Mambo hayo yatakapotokea, nitawavuta watu wote waje kwangu.” 33 Yesu alisema hili kuonesha jinsi ambavyo atakufa.

34 Watu wakasema, “Lakini sheria yetu inasema kwamba Masihi ataishi milele. Sasa kwa nini unasema, ‘Ni lazima Mwana wa Adamu ainuliwe juu’? Ni nani huyu ‘Mwana wa Adamu’?”

35 Kisha Yesu akasema, “Nuru[h] itabaki pamoja nanyi kwa muda mfupi tu. Kwa hiyo mtembee mkiwa bado na hiyo nuru. Hapo giza[i] halitaweza kuwakamata. Watu wanaotembea gizani hawajui kule wanakoenda. 36 Hivyo wekeni matumaini yenu katika nuru wakati bado mkiwa nayo. Jinsi hiyo mtakuwa watoto wa nuru.” Yesu alipomaliza kusema mambo hayo, aliondoka na kwenda mahali ambapo watu wasingeweza kumwona.

Baadhi ya Wayahudi Wakataa Kumwamini Yesu

37 Watu wakaona ishara[j] hizi zote alizozifanya Yesu, lakini bado hawakumwamini. 38 Haya yalikuwa hivyo ili kuthibitisha yale aliyoyasema nabii Isaya kuwa:

“Bwana, ni nani aliyeamini yale tuliyowaambia?
    Ni nani aliyeziona nguvu za Bwana?”(C)

39 Hii ndiyo sababu watu hawakuweza kuamini. Kwani Isaya alisema pia,

40 “Mungu aliwafanya baadhi ya watu wasione.
    Aliufunga ufahamu wao.
Alifanya hivi ili wasiweze kuona kwa macho yao
    na kuelewa kwa ufahamu wao.
Alifanya hivyo ili wasiweze kugeuka
    na kuponywa.”(D)

41 Isaya alisema hivi kwa sababu aliuona ukuu wa Mungu[k] ndani ya Yesu. Naye alizungumza habari zake Yesu.

42 Lakini watu wengi wakamwamini Yesu. Hata wengi miongoni mwa viongozi wa Wayahudi wakamwamini, lakini walikuwa na hofu juu ya Mafarisayo, hivyo hawakusema kwa uwazi kwamba wameamini. Hao walikuwa na hofu kwamba wangeamriwa watoke na kukaa nje ya sinagogi. 43 Wao walipenda kusifiwa na watu zaidi kuliko kupata sifa zinazotoka kwa Mungu.

Mafundisho ya Yesu Yatawahukumu Watu

44 Kisha Yesu akapaza sauti, “Mtu yeyote anayeniamini basi kwa hakika anamwamini yule aliyenituma. 45 Yeyote anayeniona mimi hakika anamwona yeye aliyenituma. 46 Nimekuja katika ulimwengu huu kama mwanga. Nimekuja ili kila mmoja atakayeniamini asiendelee kuishi katika giza.

47 Sikuja ulimwenguni humu kuwahukumu watu. Nimekuja ili kuwaokoa watu wa ulimwengu huu. Hivyo mimi siye ninayewahukumu wale wanaosikia mafundisho yangu bila kuyafuata. 48 Isipokuwa yupo hakimu wa kuwahukumu wote wanaokataa kuniamini na wasiokubaliana na yale ninayoyasema. Ujumbe ninaousema utawahukumu ninyi siku ya mwisho. 49 Hiyo ni kwa sababu yale niliyofundisha hayakutoka kwangu. Baba aliyenituma ndiye aliyeniambia yale nitakayosema na kuyafundisha. 50 Nami najua amri za Mungu kwamba lolote alisemalo na kutenda litawaletea watu uzima wa milele, kama watazifanya. Hivyo mambo ninayosema ni yale ambayo Baba yangu ameniambia niyaseme.”

Footnotes

  1. 12:3 nusu lita Kwa maana ya kawaida, “litra” ni ratili ya Kirumi, sawa na gramu 327.
  2. 12:5 mshahara wa mwaka Wa mwaka wa mtu kwa hali halisi “dinari 300” (sarafu za fedha). Sarafu moja, dinari ya Kirumi, ilikuwa ni wastani wa mshahara wa mtu wa siku moja.
  3. 12:8 maskini Nyakati zote wataendelea kuwepo maskini pamoja nanyi. Tazama Kum 15:11.
  4. 12:13 Msifuni Kwa maana ya kawaida, “Hosanna”, ambalo ni neno la Kiebrania lililotumika kumwomba msaada Mungu. Hapa, labda ilikuwa ni kelele ya shangwe iliyotumika kumsifu Mungu au Masihi wake.
  5. 12:15 watu wa Sayuni Kwa maana ya kawaida, “binti Sayuni”, ina maana mji wa Yerusalemu. Tazama Sayuni kwenye Orodha ya Maneno.
  6. 12:31 mtawala wa ulimwengu Huyu ni Shetani. Tazama Shetani katika Orodha ya Maneno.
  7. 12:32 nitainuliwa juu Hapa “Kuinuliwa juu” ina maana ya kupigiliwa misumari msalabani na “kuinuliwa” nao. Pia katika mstari wa 34.
  8. 12:35 Nuru Ina maana ya Kristo, kama katika Yh 1:5-9. Pia ni ishara ya wema na kweli unahusiana na Kristo na ufalme wake.
  9. 12:35 giza Giza au usiku ni ishara ya aina zote za mambo yanayoueleza ufalme wa Shetani, kama vile dhambi na maovu.
  10. 12:37 ishara Ni tendo la kushangaza linalodhihirisha nguvu za Mungu.
  11. 12:41 Mungu Kihalisia, “utukufu”, ni neno linaloonyesha sifa maalumu za Mungu. Tazama Utukufu katika Orodha ya Maneno.